Nafasi Ya Matangazo

April 25, 2016

Rais  wa  VICOBA Devotha Likokola amewaasa  wafanyakazi waliopo kwenye ajira hususani wanawake  kujiunga na vikundi vya VICOBA ili waweze kujikwamua kimaisha na kuboresha maisha ya familia zao.

Bi.Likokola alitoa wito huu jana wakati wa mafunzo ya ujasiriamali kwa wanawake wanaofanya kazi katika kampuni ya DarBrew inayotengeneza kinywaji cha Chibuku iliyofanyika katika kiwanda cha Dar es Salaam.

Alisema kwa kujiunga na VICOBA wanawake hao watakuwa na uwezo wa kupata mikopo yenye masharti nafuu na kupata mafunzo ya fursa mbalimbali za kibiashara zilizopo na kuwakutanisha na wanawake wenzao ili waweze kubadilishana uzoefu wa maisha.

“Kuna dhana kwamba VICOBA ni kwa ajili ya akina mama wasio na ajira na wanawake wengi walioajiriwa kutotaka kujiunga na vikundi  hivi kwa ajili ya kuwakwamua  kiuchumi matokeo yake  waajiriwa wengi wanaachwa nyuma kiuchumi kutokana na kutegemea mshahara wa mwisho wa mwezi tu”.Alisema Likokola.

Aliwaasa wanawake  kuchangamkia fursa hii  ambayo pia imeanza kuchangamkiwa na wanaume na kuwataka waajiri  kuwezesha wafanyakazi wao kupata mafunzo ya ujasiriamali ili yawaandae kujiajiri baada ya muda wao wa ajira kumalizika na hata wakiwa makazini bado kuna shughuli mbalimbali za ujasiriamali wanaweza kuzifanya kwa ajili ya kuinua vipato vyao.

Katika mafunzo hayo wanawake wafanyakazi wa DARBREW walipatiwa mwongozo wa kujiunga na vikundi vya VICOBA ambapo pia walipatiwa elimu ya ujasiriamali,jinsi ya kuibua miradi na kuiendesha pia walipatiwa ushauri wa jinsi ya kutumia fedha kwa malengo ya kufanikiwa na umuhimu wa kujiwekea akiba.

VICOBA ambayo ilianzishwa ikiwa na mtizamo wa kusaidia vikundi vya wanawake wa vijijini kiuchumi imezidi kupanua huduma kwa wanawake wengi nchini ambapo hivi sasa inao mtandao wa vikundi zaidi ya 10,000 nchi nzima vyenye wanachama zaidi ya 500,000 na mtaji unaofikia  zaidi ya  shilingi bilioni 75
Rais wa Vicoba endelevu Tanzania, Devotha Likokola, akitoa  mafunzo ya elimu ya vicoba kwa wafanyakazi wa Kiwanda cha Chibuku (Darbrew Ltd) cha Ubungo jijini Dar es Salaam.
 Mratibu wa Vicoba  mkoa wa Dar es Salaam, Amina Mkuwa (kulia)  akigawa vipeperushi vya taasisi hiyo wakati wa mafunzo hayo.
Wafanyakazi wa Chibuku (Darbrew Ltd)Ubungo jijini Dar es Salaam, wakiwa katika picha ya  pamoja na Rais wa Vicoba endelevu Devotha Likokola mara baada ya kumalizika kwa  mafunzo.
Baadhi ya wafanyakazi wa  kiwanda cha Chibuku (Darbrew Ltd) wakisoma katiba ya Vicoba
Posted by MROKI On Monday, April 25, 2016 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo