Nafasi Ya Matangazo

November 27, 2015

 Mbunge wa Dodoma mjini, Anthony Mavunde akitembezwa katika mabweni ya shule hiyo ya Wasichana Msalato mkoani Dodoma. Pichani Mavunde akiwa katika wodi ya zahanati ya shule ambayo ilinunuliwa magodoro na mashuka.
Mbunge akitembezwa maeneo ya shule.
Umoja wa wanafunzi waliohitimu katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Msalato (Msalato alumnae) iliyoko mkoani Dodoma, umefanikiwa kufanya ukarabati wa sehemu ya miundombinu kwenye mabweni mawili ya Mandela na Moringe Ukarabati huo umegharimu takribani Shilingi milioni 8.8 zilizotokana na michango ya wana umoja kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Ukarabati umehusisha kazi zifuatazo:
Kuweka vigae (tiles) na kupaka rangi vyumba 14 vya vyoo vya mabweni ya Moringe na Mandela.

Kufufua mfumo wa majitaka kwenye vyoo vya mabweni hayo,Kuweka milango vyoo 14 na kupaka rangi.

Kununua na kuweka masinki 14 ya vyoo kwenye mabweni. Kati ya masinki hayo, 12 ni ya vyoo vya kuchuchumaa na mawili (2) ni vyoo vya kukaa kwa ajili ya wanafunzi wenye ulemavu na wasiojiweza. Kuweka mfumo wa kuingiza maji safi mabweni hayo ya Moringe na Mandela,ukarabati wa Zahanati ya Shule.  BOFYA HAPA KUSOMA ZAIDI
Maeneo mengine ni ukarabati wa matangi ya kusukuma maji. Pia tumetengeneza mfumo wa maji taka wa bweni la Moringe na kuelekeza maji ya mvua yaliyokuwa yanatuama na kuingia ndani ya chemba za maji taka na kurudi vyooni. Hii ilikuwa inasababisha vyoo kutokuwa kwenye hali ya kutumika kwani vilikuwa vinajaa maji taka.

Hii imehusisha kunyanyua chemba za maji machafu yawe usawa usioweza kuingiza maji ya mvua na pia tumefanikiwa mfereji wa kupitisha maji ya mvua yaliyokuwa yanatuama nyuma ya bweni la Moringe.

Upande wa zahanati tumefainikiwa kununua magodoro mapya kwa ajili ya mpumziko ya wagonjwa, kurekebisha vitanda ambavyo vilishakuwa vibovu, kununua mashuka, mito na foronya zake.

Msalato Alumnae inaundwa na wanafunzi waliohitimu miaka tofauti tangu Shule ya Wasichana Msalato ilipoanzishwa mwaka 1962. Kwa mapenzi mema na kuthamini kile ambacho nchi imetenda kwa kila mmoja wetu kwa kutupatia nafasi kusoma kwenye shule hii ya vipaji maalumu, tuliamua kuunda umoja uliowezeshwa na mitandao ya kijamii hususani Facebook na Whatsapp. 

Baada ya umoja huo kuundwa kwa lengo la kufahamiana na kukumbushana mambo mbalimbali ya shuleni bila kujali mwaka wa kuhitimu, liliibuliwa wazo la kuchangia maendeleo ya shule yetu. Wana Msalato Alumnae wapatao 60 tulihamasishana kila mmoja kuchangia kadri awezavyo. 

Lakini pia miongoni mwetu, wapo waliotafuta wadau kufanikisha lengo letu la kusaidia shule yetu. Juhudi hizo zilifanikisha kupata jumla ya shilingi milioni 13.5 ambazo kati yake, Sh. 5 milioni zilitoka Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) lililotuunga mkono baada ya kuwasilisha maombi yetu kwao.

Fedha iliyotolewa na TANAPA iliingia moja kwa moja kwenye akaunti ya Shule ya Wasichana Msalato. Fedha hii imehifadhiwa tukilenga kuitumia kwa ukarabati zaidi wa mabweni mengine.

Jumla ya shilingi milioni 8.8 zilizotokana na michango ya wana Msalato Alumnae ndizo zimetumika kukarabati miundombinu hiyo ya mabweni ya Moringe na Mandela chini ya usimamizi wetu. Hatua hiyo ya kukarabati maeneo husika, ilifanyika baada ya kuwasiliana na uongozi wa shule na kuelezwa maeneo yenye uhitaji mkubwa ya kukarabatiwa.

Wito wetu:
Wana Msalato Alumnae tunatoa wito kwa jamii kujenga moyo wa kujitolea kwa ajili ya maendeleo ya jamii hususani katika Nyanja za elimu na afya. Tunaendelea kuhimiza watu wote waliohitimu Shule ya Wasichana Msalato kujitolea kwa ajili ya maendeleo ya shule yetu, kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.
Posted by MROKI On Friday, November 27, 2015 1 comment

1 comment:

  1. Bigup all ladies, kwa kidogo tulichonacho tumeweza kumsaidia mtoto wa kike kukaa sehemu safi na salama...member Msalato Alumnae

    ReplyDelete

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo