Nafasi Ya Matangazo

September 04, 2015

Kocha Mkuu wa Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro, Charles Mkwasa amesema kikosi chake kipo tayari kwa mchezo wa kesho dhidi ya Nigeria kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika mwaka 2017.

Akiongea na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa mikutano wa TFF uliopo Karume, Mkwasa amesema vijana wake wapo katika hali nzuri kuelekea kwenye mchezo huo wa kesho ambao ni muhimu kwa Taifa Stars.

“Tumefanya mazoezi kwa takribani siku kumi, vijana wako katika hali nzuri ya mchezo, uwezo waanaouonyesha mazoezini ni wa hali ya juu na unatupa matumaini ya kufanya vizuri” Alisema Mkwasa.
Aidha Mkwasa amesema katika mpira hakuna kinachoshindakana, anatambua Nigeria ni timu kubwa Afrika, wameshatwaa ubingwa wa Afrika mara tatu, lakini mpira wa sasa lolote linaweza kutokea, hivyo sisi tumejiandaa vilivyo kufanya vizuri katika mchezo huo.

Mwisho Mkwasa amesema wamejindaa vizuri kwa mchezo huo wa kesho, na kuwaomba watanzania kuja kuwapa sapoti wachezaji uwanjani kwa kuwashangilia muda wote wa mchezo, na kusema kikosi chake hakina mchezaji majeruhi hata mmoja kuelekea kwa mechi hiyo.

Mechi hiyo ya kesho jumamosi itachezeshwa na waamuzi kutoka nchini Rwanda ambao ni Louis Hakizimana (mwamuzi wa kati) Honore Simba (mwamuzi msaidizi), Jean Bosco Niyitegeka (mwamuzi msaidizi), Abdoul Karim Twagiramukiza (mwamuzi wa akiba) na kamisaaa wa mchezo ni Charles Kasembe kutoka nchini Uganda ambao wote tayari wameshawaili jijini Dar es salaam tangu jana jioni.

Tiketi za mchezo huo tayari zimeshaanza kuuzwa leo saa 4 kamili asubuhi katika vituo vya (i) Ofisi za TFF - Karume , (iii) Mbagala – Dar live, (iv) Ubungo – Oilcom, (v) Makumbusho – Stendi, (vi) Uwanja wa Taifa, (vii) Mwenge – Stendi, (viii) Kivukoni-  Feri, (ix) Posta – Luther House, (x) Big Bon – Msimbazi Kariakooo

Viingilio vya mchezo huo wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON Qaulifier 2017) kundi G itakua ni VIP A Tsh 40,000, VIP B Tsh 30,000, VIP C Tsh15,000, Rangi ya Machungwa (Orange) Tsh 10,000, na viti vya rangi ya Bluu na Kijani Tsh 7,000.

TFF inawaomba watanzania, wapenzi na wadau wa mpira wa miguu kununua tiketi za mchezo huo katika magari yaliyopo kwenye vituo vilivyotajwa ili kuondokana na tatizo la kuuziwa tiketi zisizokuwa halali.
Jeshi la Polisi nchini kwa kushirikiana na idara nyingine za kiusalama wameandaa usalama wa kutosha katika kuelekea kwenye mchezo na kuhakikisha kila mpenzi wa mpira wa miguu anaingia kushuhudia mchezo huo salama na kuondoka salama.

Mchezo huo utaanza saa 10:30 jioni kwa saa za Afrika Mashariki utachezeshwa na waamuzi kutoka nchini Rwanda ambao wanatarajiwa kuwasili leo jioni pamoja na kamisaa wa mchezo huo.

Wakati huo huo Kikosi cha wachezaji 23 cha timu ya Taifa ya Nigeria (Super Eagles) kimewasili nchini jana usiku na kufikia katika hoteli ya Kempsink iliyopo eneo la Posta ambapo leo jioni watafanya mazoezi katika uwanja wa Taifa uliopo jijini Dar es salaam.

Kikosi hicho cha Nigeria kinachoongozwa na kocha Sunday Oliseh kinawajumuisha makipa Ikeme Onoro, Ezenwa Ikechukwu, walinzi Thomas Olufemi, Balogun Aderemi, kwambe Solomon, Omeruo Keneth, Ekong William, Oboroakpo Austin, Akasi Chima, na Madu Kingsley.

Wengine ni viungo Ibrahim Rabiu, Muhamed Usman, Uzochukwu Izunna, Haruna Lukman, Nwankwo Obiora, Igboun Emeka, washambuliaji Simon Daddy, Ujah Anthony, Emenike Chinenye, Musa Ahmed, Aggreh Obus na Eduok Samuel.
Posted by MROKI On Friday, September 04, 2015 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo