Nafasi Ya Matangazo

April 28, 2015

Joto la ubunge katika jimbo la Arusha mjini limezidi kupanda mara baada ya Kada wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) mkoani Arusha,Kim Fute (pichani)  kutangaza rasmi kuwania ubunge katika jimbo hilo endapo akipewa ridhaa na chama chake kugombea. Mwandishi wetu Moses Mashalla, Anaandika kutoka Arusha.

Kim,amejitokeza kutangaza azma hiyo ikiwa ni siku chache baada ya makada wengine wa CCM ambao ni Phillemon Mollel,Victor Njau,Thomas Munisi,Deo Mtui,Godfrey Mwalusamba kutangaza nia ya kuwania jimbo hilo linashikiliwa na mbunge wake,Godbless Lema ambaye tayari ametangaza kugombea  tena.

Akizungumza na gazeti hili jijini hapa,Fute alisema kuwa amesukumwa na dhamira ya kuwania ubunge katika jimbo hilo mara baada ya kutathmini na kubaini ya kwamba jimbo hilo linakabiliwa na tatizo la  ombwe la uongozi.

Alisema kwamba amejipima vya kutosha na kubaini ya kwamba  ana sifa za kutosha za kuwawakilishi wakazi wa jimbo la Arusha mjini ambao alidai kwa muda mrefu wamekuwa wakikosa viongozi bora wa kuwawakilisha.

Kada huyo alisisitiza kwamba miongoni mwa mambo ambayo atakwenda kuyafanyia kazi pindi akifanikiwa kuwa mwakilishi wa jimbo hilo ni pamoja na kushughulikia suala la usalama wa mji wa Arusha ambalo alidai tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 mji huo umeandamwa na matukio mbalimbali kama maandamano,vurugu na mambomu.

Alisema kuwa mji wa Arusha ni mji wa kimataifa na pia una fursa nyingi kama kitovu cha utalii hapa nchini na duniani hivyo atajikita kuhakikisha anasimamia hali ya kurejea kwa usalama ili biashara hiyo  iweze kufanyika kwa uwepesi kwa kuwa inachangia pato kubwa la taifa.

“Arusha ni mji wa kimataifa na una fursa nyingi kama biashara ya utalii ambayo inachangia pato kubwa la taifa lakini usalama ni hafifu na unaharibu kwa kiasi kikubwa hivyo nitajikita kuhakikisha hali ya usalama inarejea”alisema Kim

Hatahivyo,alibainisha kwamba mbali na usalama pia atahakikisha anakutana na makundi mbalimbali ya viongozi wa dini zote,waandishi wa habari pamoja na wadau wa maendeleo jijini hapa ili kuangalia namna ya kuuweka mji wa Arusha katika hali ya utulivu.

“Tunahitaji mtu sahihi wa kuunganisha siasa na uchumi mzuri, endapo nikifanikiwa kuwa mwakilishi nitahakikisha ninakutana na makundi mbalimbali ili kujadili kwa kina changamoto zetu na kubadili fikra na mtazamo kwa wakazi wa Arusha”alisisitiza Fute
Posted by MROKI On Tuesday, April 28, 2015 No comments

0 comments:

Post a Comment

  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo